Wakati tukielekea mwisho wa mwaka 2017, Jeshi la Polisi limeeleza matukio matatu kuwa ndiyo yaliyovuta hisia za jamii mwaka huu mkoani Tabora
Matukio hayo ni kuuawa kwa aliyekuwa Diwani wa Muungano, wilayani Urambo, Francis Kasanga, kuuawa kwa wanawake watano wa Kijiji cha Undomo (Nzega) na kunusurika kuuawa kwa wanawake wanne, Kijiji cha Mwamabondo (Uyui).
Kamanda wa polisi mkoa wa Tabora, Wilbrod Mutafungwa alisema matukio hayo matatu ndiyo yalivuta hisia kubwa za watu na jeshi lake kufanya kazi kwa weledi mkubwa.
Katika tukio la kuuawa kwa Kasanga, Kamanda Mutafungwa alisema diwani huyo alidungwa sindano ya sumu na kisha kufungwa kamba shingoni na kutundikwa ili ionekane amejinyonga.
Alieleza kuwa tukio hilo lililotokea Julai 7 mwaka huu, limehusishwa na mambo ya kisiasa na watuhumiwa wamekamatwa na kufikishwa mahakamani.
Katika tukio la Undomo, Kamanda Mutafungwa alisema Julai 25 kwenye kitongoji cha Mwisulu, kata ya Uchama wilayani Nzega kulifanyika mkutano wa wananchi wa eneo hilo lengo likiwa ni kuwataja na kuwabaini watu wanaojihusisha na vitendo vya kishirikina.
Alieleza kuwa mkutano huo uliongozwa na Mtemi wa Sungusungu, watu watano ambao ni wanawake walipelekwa katika mkutano huo huku wakishambuliwa kwa kupigwa fimbo sehemu mbalimbali za miili yao.
Alieleza kuwa wanawake hao baadaye walipelekwa porini kisha kuuawa na miili yao kuchomwa moto huku watuhumiwa 38 wakifikishwa mahakamani.
Katika tukio la Mwamabondo la Septemba 17 mwaka huu kata ya Loya wilayani Uyui, wanawake wanne, Manugwa Lutema, Elizabeth Kashindye, Rahel Mukowangwa na Maria Sahani walikamatwa na wananchi waliojichukulia sheria mkononi kwa tuhuma kuwa wanajihusisha na vitendo vya kishirikina.
Wanawake hao walishambuliwa kwa kupigwa maeneo mbalimbali ya miili yao kwa kutumia fimbo, kufungwa vitambaa usoni na baadaye kuwarundikia nyasi na kuni kwa lengo la kuwateketeza kwa moto.
Kabla hawajachomwa moto taarifa zilifika polisi waliochukua hatua na kufanikiwa kuwaokoa wakiwa wamejeruhiwa sehemu mbalimbali za miili yao.
Watuhumiwa 55 walifikishwa mahakamani.
Katika kipindi cha mwaka huu, watuhumiwa 201 wa mauaji, walifikishwa mahakamani kwa tuhuma za unyang’anyi wa kutumia silaha.
Katika hatua nyingine, mkoa wa Tabora umekuwa na ongezeko la makosa ya jinai kutoka makosa 16,872 mwaka uliopita hadi makosa 17,882 mwaka huu (Januari hadi Novemba) likiwa ni ongezeko la makosa 1,010 sawa na asilimia 5.98.
Alitaja makosa yaliyoshika kasi kuripotiwa kuwa ni ya kimaadili ambayo ni 602 ukilinganisha na mwaka jana yaliyokuwa 373 ikiwa ni ongezeko la makosa 229 sawa na asilimia 61.39.
Kwa upande wa makosa ya kuwania mali yaliyoripotiwa mwaka huu ni 1,215 ukilinganisha na 1,417 mwaka jana, hivyo kuwa na upungufu wa makosa 202 sawa na asilimia 14.25.
Makosa dhidi ya binadamu yaliyoripotiwa mwaka huu ni 404 ukilinganisha na mwaka jana yaliyokuwa 431 mwaka jana ambayo ni pungufu ya makosa 27 sawa na asilimia 6.26.
“Ongezeko la makosa hayo linatokana na juhudu za askari kufanya operesheni, misako na doria katika maeneo mbalimbali mkoani Tabora,” alisema Mutafungwa.
Pamoja na hayo, polisi mkoani Tabora pia imeongeza makusanyo kutokana na adhabu za barabarani kwa zaidi ya Sh600 milioni katika kipindi cha mwaka mmoja.
Kiasi hicho kimetokana na makosa ya usalama barabarani yapatayo 55,081 hadi Novemba mwaka huu ukilinganisha na makosa 34,540 ya mwaka jana, hivyo kuwa na ongezeko la makosa 20,541 sawa na asilimia
Admit Mwananchi