Maagaidi wakufurishaji wa kundi la ISIS au Daesh wamehujumu kituo cha polisi katika mji wa bandarini wa Aden kusini mwa Yemen na kuuawa watu 14.
Kwa mujibu wa maafisa wa tiba katika hujuma hiyo ya Jumamosi iliyojiri katika mtaa wa Tawahi kusini magharibi mwa Aden, watu wengine 40, wakiwemo wanawake na watoto walijeruhiwa.
Kundi la kigaidi la ISIS lilitangaza kuhusika na jinai hiyo ambayo ilijumuisha magari mawili yaliyokuwa yamesheheni mabomu.
Hujuma hiyo ni ya kwanza ya aina yake tokea mwezi Januari wakati yalipojiri mapigano makali baina ya wanamgambo wanaotaka kujitenga eneo la kusini mwa Yemen na wafuasi wa rais wa zamani wa nchi hiyo Abdu Rabbu Mansour Hadi wanaoudhibiti mji huo.
Machafuko hayo yalijiri baada ya wanaotaka kujitenga kufanikiwa kudhibiti kambi kadhaa za kijeshi zilizokuwa zikisimamiwa na mrengo wa Hadi. Duru zinadokeza kuwa wanaotaka kujitenga kusini mwa Yemen wanaungwa mkono na Umoja wa Falme za Kiarabu huku Saudi Arabia ikiripotiwa kuunga mkono mrengo wa Hadi.
Mji wa bandarini wa Aden una umuhimu wa kistratijia na kwa msingi huo inatazamiwa malumbano ya kuwania mji huo yataendelea huku Yemen ikiendelea kushuhudia hujuma ya kila siku ya ndege za kivita za Saudia.
Saudia kwa kusaidiwa na Marekani, Israel na baadhi ya nchi za Kiarabu ilianzisha mashambulizi ya kila upande dhidi ya Yemen tangu mwezi Machi mwaka 2015 kwa lengo la kumrejesha madarakani kibaraka wake, Abdrabbuh Mansur Hadi rais wa zamani wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kisha kukimbilia Saudia.
Hata hivyo licha ya njama hizo hadi sasa Saudia na washirika wake wameshindwa kufikia malengo yao ndani ya Yemen.
No comments:
Post a Comment