Wednesday, October 25, 2017

25 October 2017, Rais wa Msumbiji awatumbua wakuu wa upelelezi na majeshi

Rais wa Msumbiji amewafuta kazi Mkuu wa Shirika la Upelelezi na Mkuu wa Majeshi ya nchi hiyo wiki mbili baada ya mauaji ya watu 16 katika shambulizi lililofanyika kaskazini mwa nchi hiyo.

Taarifa iliyotolewa jana na Rais Filipe Jacinto Nyusi imesema kuwa, Mkurugenzi Mkuu wa Upelelezi na Huduma za Usalama, Lagos Lidimo amefutwa kazi na nafasi yake itachukuliwa na Julio Jane aliyekuwa kamanda wa polisi ya nchi hiyo.

Imeongeza kuwa Mkuu wa Majeshi ya nchi hiyo, Graça Chongo pia ameachishwa kazi.

Hata hivyo ripoti hiyo haikuainisha nani atachukua nafasi hiyo.

Taarifa ya Rais wa Msumbiji haikutaja sababu ya kufutwa kazi maafisa hao wa juu wa masuala ya upelelezi na jeshi.

Mapema mwezi huu polisi ya Msumbiji ilikabiliana na watu waliokuwa na silaha katika bandari ya Mocimboa da Praia katika Bahari ya Hindi ambapo watu 16 waliuawa wakiwemo maafisa wawili wa jeshi la polisi.

Haikujulikana mara moja sababu ya mapigano hayo wala utambulisho wa watu waliokuwa wakipigana na polisi.

No comments: