Mwakilishi wa kamisheni kuu ya Korea Kaskazini katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, ni suala linalowezekana sana kutokea kwa vita vya nyuklia katika Rasi ya Korea, kutokana na kuendelea maneva ya kijeshi ya Marekani na Korea Kusini katika eneo hilo.
Kim In-ryong ameyasema hayo katika hali ambayo Marekani na Korea Kusini zinaendelea na maneva ya kijeshi ya siku tano katika eneo hilo.
Inaelezwa kuwa, maneva hayo ni kati ya maneva makubwa zaidi kufanywa na Washington na Seoul.
In-ryong ambaye pia ni naibu balozi wa Korea Kaskazini katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Korea ni nchi pekee duniani ambayo tangu mwaka 1970 imekuwa ikilengwa moja kwa moja na Marekani kwa kila aina ya vitisho.
Akiendelea amesema kuwa, maadamu siasa za uhasama za Marekani zitaendelea dhidi ya nchi yake, Pyongyang kamwe haitositisha kwa aina yoyote miradi ya silaha zake za nyuklia na makombora ya balestiki.
Katika hatua nyingine Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea Kusini amesisitizia udharura wa ushirikiano wa karibu sana wa nchi yake, Marekani na Japan kwa ajili ya kile alichokisema kuwa ni kukabiliana na Korea Kaskazini.
Kang Kyung-hwa alisema hayo jana (Jumatano) alipokutana na Shinsuke Sugiyama, naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan mjini Seoul na kuongeza kuwa, ushirikiano huo wa nchi tatu utasaidia kujadiliwa hatua zinazopaswa kuchukuliwa dhidi ya Pyongyang ikiwemo vikwazo.
Naye John Sullivan Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani amefanya safari nchini Korea Kusini ambako amekutana na kufanya mazungumzo marefu na viongozi wa nchi hiyo kuhusiana na Korea Kaskazini.
No comments:
Post a Comment