Wakazi wa mji wa Bukavu, katikati ya mkoa wa Kivu Kusini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamefanya maandamano makubwa kulalamikia machafuko yanayoendelea katika mkoa huo.
Katika maandamano hayo inaelezwa kuwa mtu mmoja amefariki na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya kufyatuliwa risasi na polisi wa serikali.
Habari zinaarifu kwamba, maandamano hayo yaliyofanyika katika eneo la watu masikini la Panzi, mjini Bukavu yalikabiliwa na polisi wa kutuliza ghasia ambapo imetangazwa kuwa mtu aliyeuawa kwa kupigwa risadi ni mwanafunzi aliyekuwa na umri wa miaka 14.
Watu walioshuhudia wamesema kuwa, waandamanaji sambamba na kuchoma moto matairi ya magari, walifunga barabara sambamba na kukitia moto kituo kidogo cha polisi cha eneo hilo la Panzi.
Awali uongozi wa kata ya Mwenga ya mkoa wa Kivu Kusini, ilitangaza habari ya kutoroka jela wafungwa 34 kutoka jela ya katikati ya eneo hilo, Jumapili iliyopita ambapo polisi ilifanikiwa kuwatia mbaroni wafungwa watatu kati yao.
Machafuko na ukosefu wa amani vinaendelea kushuhudiwa katika maeneo ya mashariki na kaskazini mwa Kongo kwa zaidi ya miaka ishirini sasa.
Kushindwa jeshi na kikosi cha wanajeshi wa Kofia Bluu wa Umoja wa Mataifa kuwaangamiza wanamgambo kumezidisha hali ya mchafukoge mashariki mwa nchi hiyo.
No comments:
Post a Comment